Wimbo wa kwanza Mwili Wangu Ni Mwili Wangu
Lengo la Wimbo
Kuwafunza watoto kuwa mwili wao ni wao na hakuna aliye na haki ya kumuumiza wala kumshika sehemu zake za siri.
Mojawapo ya jambo la kwanza kuwaeleza watoto ni kuwa miili yetu ni maalum, na hakuna aliye na haki ya kutuumiza wala kuzishika sehemu zetu nyeti. Kisha dhihirisha ziliko sehemu hizo nyeti- ni sehemu za mwili wao ambazo zimefichwa kwa mavazi ya ndani, ni sehemu za siri na ni zao pekee yao.
Sasa ni muhimu pia kuwaeleza watoto kuwa kunao wakati ambao wazazi au watunzaji wao watazigusa sehemu zao za siri kama vile:-
1) Wanapokuwa wachanga, kunaye atakayemwosha, lakini wanapoendelea kukua
watajua jinsi ya kunawa wenyewe.
2) Wazazi au watunzaji huenda wakahitajika kuwapaka dawa katika sehemu zao za
siri endapo mto yu mgonjwa au ana maumivu. Hakikisha kwamba wamefahamu kuwa
hili ni jambo la kufanywa tu na wazazi, watunzaji au madaktari, na iwapo watahisi kwamba haliwafurahishi wanaweza kufunzwa jinsi ya kujipa dawa wenyewe.
3) Huenda daktari akahitajika kuzishika sehemu zao za siri endapo wanaugua au
wana maumivu, ila Mama, Baba au Mtunzaji atakuwepo kila wakati endapo
daktari atahitajika kumshika sehemu hizo.
Mwili Wangu
Ni
Mwili Wangu
Bure Muziki Kuzuia
Watoto Kuzuia
Programu
Hakuna wakati mwingine wowote ambao mtu yeyote anafaa kuzishika sehemu zao za siri. Watoto wanajua kuwa ni vyema kusema “Hapana” endapo mtu atawafanya washikwe na wasi wasi au akidhubutu kuwashawishi wafanye
vitendo wanavyojua ni hatia.ь.
Zaidi ya asilimia 90% ya dhulma za kingono hufanyika kati ya jamaa au hutekelezwa na mtu ajulikanaye na kuaminiwa na mtoto mhusika. Ni jambo ambalo humwangamiza mtoto uaminifu wake unaposalitiwa. Wanastahilii kujua kwamba wana pahali pema pa kuenda kuomba usaidizi na mtu atakayewasikiliza na kuwaamini.
Kueka Siri
Wanyanyasaji watoto na wanaodhulumu watoto kingono kwa mara nyingi hutegemea maarifa kuwa watoto wataweka siri na kwa sababu hii pekee ni jambo zuri kuwa na sheria ya “kutokuwa na siri”. Kuwaelimisha watoto hawa tangu utotoni mwao kutawafanya wahisi vyema kutoweka siri “hatari” iwapo kuna mtu anayewaumiza au kuwashika kwa njia isiyofaa.
Watoto wanafaa kujulishwa kuwa iwapo watadhulumiwa:
-
Hawana lolote la kulaumiwa
-
Hawastahili kuhisi vibaya
3) Ni vyema kusema ili dhulma hiyo ikomeshwe
Tafadhali kumbuka kuwa mwenye kutekeleza unyama huo kwa mara nyingi huwa ni mtu ambaye anapendwa na mtoto huyo ama anayejulikana na kuaminiwa naye, hivyo basi suala hili linafaa kujadiliwa kwa utaratibu mwingi.
Usiwe mwenye hasira mbele ya mtoto huyo, anakuhitaji uwe mtulivu na uweze kudhibiti hali hiyo.
Unaweza kumwelezea kuwa kwa njia sawa na walivyo waraibu wa dawa za kulevya au mraibu wa pombe, watu ambao huwadhulumu watoto wanahitaji usaidizi. Kwa njia hii wanaweza kubadili mienendo yao na kutowaumiza watoto tena. Ni kwa sababu hii ni jambo muhimu sana wao kumwambia mtu.
Umri wa kidijitali
Katika umri huu wa kidijitali, tunafaa kuwalinda watoto kutokana na watu walio na nia ya kuwapiga picha zisizofaa. Unapowazungumzia kuhusu kushikwa kwa njia isiyofaa, pia unafaa kutaja kuwa huenda watu wakataka kuzipiga sehemu zao za siri picha (hata kama hawatajaribu kuwashika kwa njia isiyofaa) na endapo
mtu atajaribu kuwapiga picha ni lazima waseme HAPANA! na kisha kumwambia mtu.

Nakala ya Cynthie toka kwenye video
Hamjambo, jina langu ni Cynthie na leo tutafanya mpango wa “Mwili wangu ni Mwili wangu”. Tutaimba nyimbo kadhaa, tufurahie na tusome kuhusu jinsi ya kukaa salama.
Mnajua, miili yetu ni maalum sana na hakuna mtu anayefaa kutuumiza, ama kushika sehemu zetu za siri ama kufanya jambo lolote la kutupatia wasiwasi kwa sababu ni mwili wetu maalum.
Tutaimba wimbo wetu wa kwanza sasa –
na nataka pia nanyi muimbe pamoja na mimi –
Unaitwa mwili wangu ni mwili wangu
Mwili wangu ni Mwili Wangu (wimbo)
Ni mwili wangu, mwili wangu,
na hakuna mtu aliye na haki ya kuniumiza
Kwa sababu mwili wangu ni mwili wangu kwangu
Ni mwili wangu, mwili wangu
na hakuna mtu aliye na haki ya kunigusa
Kwa sababu mwili wangu ni wangu kwangu
Nina mikono miwili ya kuhisi, na macho mawili ya kuona
Na masikio mawili ya kusikia unachoniambia
Nina miguu miwili yenye nguvu ya kunipeleka kwenye naenda
Na pia nina sehemu za siri ambazo sitaki kuonyeshana
Ni mwili wangu, mwili wangu na hakuna mtu aliye na haki ya kuniumiza
Kwa sababu mwili wangu ni wangu, na hakuna mtu aliye na haki ya kunigusa
Kwa sababu mwili wangu ni wangu kwangu
Nina nywele kichwani mwangu nataka uzione Na kitovu kidogo katikati yangu
Na pua rembo na vidole kumi vidogo
Na nina mdomo wa kukuambia ninachotaka ujue
Ni mwili wangu, mwili wangu
Na hukuna mtu aliye na haki ya kuniumiza
Kwa sababu mwili wangu ni mwili wangu kwangu
Ni mwili wangu, mwili wangu
Na hakuna mtu aliye na haki ya kunigusa
Kwa sababu mwili wangu ni mwili wangu kwangu Ndiyo,
Mwili wangu ni mwili wangu kwangu

Nakala hii imeandikwa na kuhuishwa na
Chrissy Sykes © 2017
Rekodi na: Thierry Irambona
Tafsiri : JB Mugi
Music Studio Sponsored by Stichting GetOn